Breaking News

WANAZUONI WAHIMIZA WAISLAMU KUTOA ZAKA KUPAMBANA NA UMASKINI


Mwenyekiti wa Umoja wa Wanazuoni wa Kiislamu, Sheikh Abdallah Swallehe Ndauga.

***
Mwenyekiti wa Umoja wa Wanazuoni wa Kiislamu, Sheikh Abdallah Swallehe Ndauga, amewahimiza Waislamu kutekeleza ipasavyo ibada ya Zaka ili kusaidia kupunguza umasikini katika jamii.

Akizungumza katika kongamano la wanazuoni wa Kiislamu lililofanyika katika ukumbi wa Dar es Salaam Youth Centre (DYCC) jijini Dar es Salaam, Sheikh Ndauga alisema Zaka ni moja ya ibada muhimu inayolenga kuwasaidia watu wenye uhitaji katika jamii.
Mwenyekiti wa Umoja wa Wanazuoni wa Kiislamu, Sheikh Abdallah Swallehe Ndauga.


Alisema kwa mujibu wa mafundisho ya dini ya Kiislamu, Zaka imewekwa mahsusi ili kuwainua watu wasiojiweza pamoja na kuimarisha mshikamano wa kijamii miongoni mwa waumini wa dini hiyo.


Sheikh Ndauga alieleza kuwa Waislamu wakitekeleza ibada hiyo kwa uaminifu na kwa kuzingatia maelekezo ya dini, inaweza kuwa nyenzo muhimu ya kupunguza umasikini na kuboresha maisha ya watu wengi.


Kwa upande wake, Sheikh Ally Zuberi akichangia mada katika kongamano hilo, alisema kumekuwepo na dhana potofu miongoni mwa baadhi ya Waislamu kuhusu walengwa wa Zaka.

Alisema baadhi ya watu wamekuwa wakidai kuwa Zaka inapaswa kutolewa kwa yatima pekee bila kuzingatia mafundisho sahihi ya Kiislamu kuhusu makundi yanayostahili kupewa Zaka.


Sheikh Zuberi alifafanua kuwa katika mafundisho ya Kiislamu, yatima hawakutajwa moja kwa moja miongoni mwa makundi ya wanaostahili kupewa Zaka isipokuwa pale wanapokuwa katika hali ya umasikini.


Wanazuoni hao walisisitiza umuhimu kwa Waislamu kujifunza na kuelewa kwa usahihi mafundisho ya dini kuhusu utoaji wa Zaka ili kuhakikisha ibada hiyo inatekelezwa kwa mujibu wa utaratibu uliowekwa.

















from MALUNDE 1 BLOG https://ift.tt/Tmep2ti

No comments