CHAMA CHA WANUNUZI NA WAUZAJI MADINI WAMLILIA MAGUFULI,WATOA SALAMU ZA POLE KWA RAIS SAMIA
Na Woinde Shizza , Michuzi Tv -Arusha
Akiongea na vyombo vya habari ofisini kwake mwenyekiti wa TAMIDA Taifa,Sammy Mollel ameeleza kwamba TAMIDA imeshitushwa na kifo cha hayati Magufuli kwani alikuwa mwamba aliyefanikiwa kuzalisha mabilionea kupitia sekta ya Madini.
Alisema kuwa Magufuli alifanikiwa kudhibiti utoroshwaji wa madini kwa kujenga ukuta Mererani,Kuanzisha masoko ya madini Nchi nzima na hivyo kupelekea kuongezeka kwa pato la taifa kupitia sekta hiyo.
"Sisi wafanyabiashara wa Madini TAMIDA tunatoa pole kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Samia Suluhu Hassan kwa kuondokewa na hayati John Magufuli kwani tunakumbuka mageuzi makubwa yaliyofanywa na serikali yake katika sekta ya Madini"alisema
Mollel ameeleza kuwa TAMIDA inakumbuka jinsi hayati Magufuli alivyochangia kulipaisha Taifa kiuchumi hadi kufikia uchumi wa Kati huku sehemu ya pato hilo la taifa likiongezeka kupitia sekta ya madini.
Aidha ameongeza kuwa Magufuli alikuwa na uwezo wa kubuni na kutekeleza miradi mbalimbali mikubwa ya kimkakati nchini ikiwemo kuboresha miundo mbinu kwa mtandao wa Lami,ujenzi wa Reli ya Kisasa (Standard Gauge).
Miradi mingine ni pamoja na kufufua shirika la ndege ATCL kwa kununua ndege 7 zikiwemo mbili kubwa Aina ya Boeing 787 ,Dreamliner na kufanikiwa kusomesha bure wanafunzi wa shule za Msingi na Sekondari .
Alisema pamoja na mafanikio hayo Hayati Magufuli alilenga kuwasaidia wanyonge wanaodhulumiwa haki zao na kusaidia wafanyabiashara wadogo wadogo kutonyanyaswa mijini.
Mwenyekiti wa TAMIDA Sammy Mollel akiongea na waandishi wa habari ofisini kwake
from MICHUZI BLOG
No comments