- Waandishi
6 wauawa kwa shambulio la anga karibu na Hospitali ya Al-Shifa
- Zaidi
ya wanahabari 240 wameuawa Gaza tangu Oktoba 2023
- Umoja
wa Mataifa wataka uchunguzi huru wa kimataifa
Na Mwandishi wetu - Dar es Salaam, Tanzania
Shirikisho la Baraza la
Vyombo vya Habari Duniani (World Association of Press Councils (WAPC)
limeilaani vikali Israel kwa kile linachokiita mauaji yaliyolengwa ya
waandishi wa habari mjini Gaza, likiutaja kuwa ni uvunjifu mkubwa wa haki za
binadamu na uhuru wa habari duniani.
Tarehe 10 Agosti 2025, shambulio la anga la Israel lilipiga
hema la waandishi wa habari karibu na Hospitali ya al-Shifa, Gaza City, na kuua
waandishi watano wa Al Jazeera Anas al-Sharif, Mohammed Qreiqeh, Ibrahim
Zaher, Mohammed Noufal na Moamen Aliwa pamoja na mwandishi wa kujitegemea
Mohammad al-Khaldi.
WAPC imesema waandishi hao walikuwa waangalizi huru
waliokuwa wakiripoti ukweli na kutoa sauti kwa raia wasio na nafasi ya
kujieleza, na si wapiganaji kama ilivyodaiwa na jeshi la Israel.
Tangu Oktoba 7, 2023, zaidi ya waandishi wa habari na
wafanyakazi wa vyombo vya habari 242 wengi wao Wapalestina wameuawa katika
mashambulizi yanayohusiana na mzozo wa Gaza. WAPC imeutaja kipindi hiki kama cha
mauaji mabaya zaidi kwa wanahabari katika historia ya kisasa, na kuongeza
kuwa hakuna mzozo mwingine umewahi kushuhudia idadi kubwa ya vifo vya
wanahabari katika muda mfupi kiasi hiki.
Mashirika ya kimataifa yameendelea kushutumu kile
kinachoelezwa kama mauaji ya mfumo dhidi ya wanahabari, uharibifu wa
miundombinu ya vyombo vya habari na vizuizi dhidi ya taarifa huru. WAPC
imesisitiza kuwa vitendo hivyo ni uvunjaji wa moja kwa moja wa sheria za
kimataifa za kibinadamu na vinatishia demokrasia ya dunia nzima.
Rais wa WAPC, David Omwoyo, amesema shirikisho hilo linaunga
mkono wito wa Umoja wa Mataifa wa kufanyika kwa uchunguzi wa kina, wa haraka na
huru wa kimataifa ili kuwawajibisha wote waliohusika. Amezitaka pande zote
katika mzozo wa Gaza kuheshimu ulinzi wa wanahabari chini ya Mikataba ya Geneva
na kusitisha mara moja mashambulizi dhidi yao.
“Hakuna nguvu za ghasia zitakazoweza kuinyamazisha kalamu,”
amesema Omwoyo. “Ukweli utashinda.”

Mwandishi Anas al-Sharif alikuwa miongoni mwa wafanyakazi watano wa Al Jazeera waliouawa na shambulio la Israel huko Gaza.

