Breaking News

Afrika yaanza safari kuwafikishia umeme wananchi milioni 300

 

 -Rais Samia ataka uunganishwaji nguvu na wadau kuhakikisha mpango huo unafikiwa  ifikapo 2030

 -Wakuu wa Nchi wasaini Azimio la Dar es Salaam lengo likiwa ni kuchochea maendeleo barani Afrika hususan ya kiuhumi, nishati

Abraham Ntambara na Tunu Bashemela



Abraham Ntambaraa na Tunu Bashemela, Dar es Salaam

WAKUU wa Nchi za Afrika wamesaini kwa pamoja tamko la Azimio la Dar es Salaam ikiwa ni mkakati wa utekelezaji wa kuwafikishia umeme wananchi milioni 300 barani Afrika.

Akizungumza kabla ya kusaini azimio hilo wakati wa Mkutano wa Wakuu wa Nchi za Afrika kuhusu Nishati ujulikanao kama “Missioni 300” mapema leo jijini Dar es Salaam Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan alisema nchi za Afrika zinapaswa kuunganisha nguvu katika kuhakikisha wananchi wake wanafikiwa na nishati ya umeme ili kuchochea ukuaji wa uchumi.

Rais Dkt. Samia alisema Tanzania imepiga hatua kwa kusambaza umeme katika vijiji vyote na sasa inaweka mkazo katika kufikisha nishati hiyo ngazi ya vitongoji.

“Mpaka sasa tumefanikiwa kuunganisha umeme katika vijiji vyote 12,318   na vitongoji 32,827 kazi inayoendelea ni kuunganisha umeme kwenye vitongoji 31,532 vilivyobakia kabla ya mwaka 2030," alisema Rais Dkt. Samia.

Rais Dkt. Samia alisema kupitia mpango wa nishati Tanzania inafanya kazi ya kuongeza uzalishaji na uimarishaji wa miundombinu ya usambazaji wa umeme akiongeza kuwa nchi za Afrika lazima ziunganishe nguvu za wadau kwa lengo la kuwafikishia nishati ya umeme wananchi milioni 300 kufikia 2030.

Aidha, alisema Tanzania inatekeleza mkakati wa Taifa wa nishati safi ya kupikia wenye lengo la kuwezesha wananchi wote kuondokana na madhara ya nishati ya kupikia isiyo safi kutoka asilimia 10 za sasa hadi 80 ifikapo mwaka 2030.

Aidha, Rais Dkt. Samia alisema Tanzania ni kitovu cha kuuza nishati ya umeme kwa nchi zinazoizunguka zikiwemo Burundi, Rwanda, Kenya huku ikiendelea kuunganisha umeme kwa nchi za Zambia na Uganda. 

Awali akizungumza wakati wa kumkaribisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuhutubia, Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati Dkt. Doto Biteko alisema Rais Dkt. Samia amesimamia agenda ya nishati safi ya kupikia kwa kuhakikisha wananchi wanafikiwa na nishati ya umeme.

Dkt. Biteko alisema Tanzania imeongeza uzalishaji wa  umeme kutoka megawati 1,888 hadi 3,431. Mkutano huo wa Wakuu wa nchi za Afrika kuhusu nishati ulihitimishwa jana Januari,2025.



No comments