Breaking News

MAJALIWA: VIONGOZI WA DINI ONGOZENI MAPAMBANO DHIDI YA MADAWA,KUDORORA MAADILI

 



KILIMANJARO: Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ametoa wito kwa viongozi wa dini kote nchini kuwa mstari wa mbele katika kuhamasisha jamii kuhusu uzingatiaji wa maadili, akisisitiza kuwa madhehebu hayo yana nafasi muhimu katika kupambana na vitendo vinavyoharibu mila na tamaduni za Kitanzania.

Akihutubia waumini na viongozi wa dini alipomwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika ibada ya kumweka wakfu Askofu Mteule Dkt. Daniel Henry Mono wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dayosisi ya Mwanga, Majaliwa alisema taifa linakabiliwa na ongezeko la matumizi na usambazaji wa dawa za kulevya, hasa miongoni mwa vijana.

“Tuendelee kupambana vikali na matumizi ya dawa za kulevya. Vijana ni kundi la msingi katika ujenzi wa taifa letu, na hatuwezi kulifumbia macho janga hili linaloharibu uelewa na afya yao,” alisema Waziri Mkuu.

Aidha, alibainisha kuwa Serikali imeendelea kuweka sheria kali dhidi ya biashara hiyo haramu sambamba na kuimarisha udhibiti mipakani, lakini bado kunahitajika msaada mkubwa kutoka kwa taasisi za kidini katika utoaji wa elimu kwa jamii.

Waziri Mkuu alitumia jukwaa hilo pia kuipongeza KKKT na madhehebu mengine kwa ushirikiano wao na Serikali katika utoaji wa huduma mbalimbali kwa jamii kama vile elimu, afya, malezi ya vijana na utunzaji wa mazingira.

“Serikali itaendelea kushirikiana na madhehebu ya dini katika masuala yote yanayolijenga taifa letu. Tushirikiane kujenga jamii ya upendo, amani na maadili mema,” alisema.

Katika hotuba hiyo, Majaliwa alitangaza kuwa Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 488 kwa ajili ya upanuzi wa barabara ya njia nne kutoka Mailisita, Kiboriloni hadi Holili – hatua itakayochochea maendeleo ya mkoa wa Kilimanjaro na kuongeza fursa za kiuchumi.

Kwa upande wake, Askofu Mteule Dkt. Mono aliwahimiza Watanzania kuendelea kuombea taifa, hasa wakati huu ambapo nchi inaelekea kwenye uchaguzi mkuu mwezi Oktoba, akisema ni muhimu kuhakikisha uchaguzi unakuwa wa haki, amani na unaozingatia mapenzi ya Mungu.

“Tutaendelea kushirikiana na Serikali kama mdau mkubwa wa maendeleo, pasipo kuvunja misingi ya imani ya Kanisa. Tunalo jukumu la kuwa sauti ya matumaini kwa taifa letu,” alisema Dkt. Mono.

Uteuzi wa Dkt. Mono umepongezwa na viongozi mbalimbali wa dini na Serikali, huku ukitambuliwa kama ishara ya kuaminiwa na jamii kutokana na hekima na maono yake ya kiroho.

 

 

No comments