Breaking News

Wapiganaji 57 wa M23 warejea nyumbani DRC

Wapiganaji 57 waliokuwa wajumbe wa kundi la waasi wa M23 wamekabidhiwa kwa serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na serikali ya Uganda.

Wapiganaji hao walioandamana na jamaa zao kumi wamesafirishwa kwa ndege ya Umoja Mataifa kutoka uwanja wa Entebbe hii leo kuelekea nchi yao.

Hatua ya kuwarejesha nyumbani imechukuliwa chini ya mpango wa utekelezaji wa makubaliano yaliofanyika mwaka 2013 ukiwa moja kati ya mikakati ya kutatua mzozo wa vita katika eneo la maziwa makuu.

Mwandishi wetu wa Kampala anasema wafuasi hao wa M23 walionekana wenye nyuso za furaha huku wakiimba kuonyesha kwamba wako tayari kurudi katika nchi yao kwa hiari .

Walimuhakikishia balozi wa Jamuhuri ya Kidemokrasia ya Kongo nchini Uganda Jean Pierre Massala kuwa wako tayari kurudi nyumbani.

Kundi hilo limekubali kurudi makwao chini ya mpango wa kuwarudisha nyumbani waliokuwa wapiganaji unaohusisha pia wapiganaji wa kundi la FDLR maarufu kama Interahamwe, linaloshutumiwa kutekeleza mauaji ya kimbari ya mwaka 1994 nchini Rwanda.

Balozi Robert Masolo ni afisa wa ngazi za juu Uganda aliyeongoza shughuli ya kuwakabidhi Wakongo hao 57 pamoja na jamaa zao 10 kwa serikali ya DRC.

Wapiganaji hao wameishi Uganda miaka mitano lakini wenzao wengi ambao idadi yao haikufichuliwa bado hawajakubali kurudishwa nyumbani chini ya mpango huo.

Wapigajani hao wamesafirishwa kwa ndege ya Umoja Mataifa.

''Watakapofika DRC watarejeshwa tena katika maisha ya kawaida'', amesema balozi wa DRC nchini Uganda Jean Pierre Massala

Bado kuna wapiganaji wengine wa zamani wa kundi la M23 eneo la Bihanga magaharibi mwa Uganda na haijulikani ni lini watarejea nyumbani kwa hiari.

from MUUNGWANA BLOG https://ift.tt/2NA6nso

No comments